Ndugai ataka Magufuli kuungwa mkono vita dhidi ya ufisadi
Spika wa Bunge, Job Ndugai akizungumza katika hafla ya kupokea taarifa za kamati maalum za bunge alizoziunda kuchanguza masuala ya gesi asilia na uvuvi wa bahari kuu, iliyofanyika jijini Dodoma leo.
Dodoma. Spika Job Ndugai amesema vita ya ufisadi aliyoianzisha Rais John Magufuli inatakiwa kuungwa mkono na kila Mtanzania, akiwataka wanaopinga kukaa sawa kwa kuwa mwendo ni uleule.
Ametoa kauli hiyo leo Jumamosi Juni 2, 2018 katika viwanja vya Bunge mjini Dodoma wakati akipokea taarifa mbili za kamati za Bunge alizoziunda kuchanguza gesi asilia na uvuvi wa bahari kuu.
Amesema baadhi ya Watanzania waliandika magazetini na baadhi ya wabunge kupinga alipounda kamati ya kuchunguza madini ya almasi na Tanzanite, ripoti zake kuwaislishwa serikalini.
Amebainisha kuwa matokeo ya kamati hizo yameanza kuonekana, ikiwamo mauzo ya madini ya Tanzanite kupanda huku akigusia jinsi ukuta kuzunguka mgodi huo ulivyojengwa.
“Kama tungekuwa sawa tusingekuwa hapa tulipo na nimpongeze Rais wetu, jambo hili si jepesi hapa tunashughulika na majitu yenye fedha nyingi, yamebaki kutununua nua tu,” amesema Spika Ndugai.
“Tumempata kiongozi, katika Ikulu yake hakuna hata mmoja anayekanyanga, lazima tumuunge mkono na wale wanaotupinga wakae sawa ila mwendo ni huo huo.”
Kuhusu mikataba, Nduigai amesema hiyo ndio yenye shida zaidi, “mikataba imetuumiza sana, hii kampuni ya Songas ni ya kinyonyaji, kupitia mikataba ya hovyo wameitishwa Tanesco mizigo ya ajabu kwa kushirikiana na kampuni ya PAP. Kampuni hizi zimeiumiza sana TPDC (Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania) kwa kuitishwa masharti ya ajabu ikiwamo kuibebesha gharama za uendeshaji.”
Akizungumzia utaratibu huo wa Bunge kuunda kamati za uchunguzi na taarifa kuwasilishwa serikalini amesema kila uongozi ana utaratibu wake na huo anaoufanya yeye anaona unafaa.
“Sisi tunafanya kazi yetu, tunakuja katika umma tunawasilisha taarifa zetu, kwa hiyo tuwapuuze watu hawa kwani hawana nia njema,” amesema.

Comments
Post a Comment