Mwanasheria Mkuu awatoa hofu wabunge
Waziri wa Katiba na Sheria, Profesa Palamagamba Kabudi akijibu baadhi ya hoja za wabunge waliochangia mjadala wa kupitisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Madini kwa mwaka wa fedha 2018/2019, jijini Dodoma leo.
Dodoma. Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Dk Adelardus Kilangi amewaondoa hofu wabunge kuhusu kushtakiwa na kufilisiwa na wawekezaji wakati wa utekelezaji wa sheria mpya za usimamizi wa madini nchini zilizofanyiwa marekebisho mwaka jana.
Akichangia bajeti ya Wizara ya Madini kwa mwaka wa fedha 2018/19, Kilangi amesema hawapaswi kuogopa kwa sababu sheria hizo zimetokana na mikataba ya kimataifa na matamko ya Baraza la Umoja wa Mataifa.
“Kuna baadhi ya watu wanasema sheria mbili zilizotungwa kuwa tumewavunja wawekezaji, sheria hizi zimetokea wapi? Lakini zimekuwepo kupitia Baraza la Umoja wa Mataifa na baadaye kuingia katika miktaba ya kimataifa.” Amesema.
Amezitaja haki kuu nne muhimu ambazo zinapatikana katika matamko ya baraza la mataifa pamoja na mikataba ya kimataifa kuwa ni haki ya nchi kumiliki maliasili, kusimamia na kudhibiti uendelezaji wa raslimali, haki ya nchi na watu wake kushiriki na haki ya nchi kunufaika na rasilimali zake.

Comments
Post a Comment